Dk. Machar chini ya kizuizi cha nyumbani katikati ya mvutano unaoongezeka

GEORGE MARATO TV
0


Vikosi vya usalama vya Nchini Sudan Kusini vimemweka Makamu wa Kwanza wa Rais na kiongozi wa upinzani Dk. Riek Machar Pamoja na Mkewe Angelina Teny ambaye ni Waziri wa Mambo ya ndani katika kizuizi cha nyumbani huko Juba huku kukiwa na mvutano wa kisiasa unaozidi kutokota na hivyo kuzua hofu na wasiwasi wa kurejea kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Sudan Kusini imekuwa na amani rasmi tangu makubaliano ya 2018 yalipomaliza mzozo wa miaka mitano kati ya vikosi vinavyomtii Rais Salva Kiir na Machar, ambao ulisababisha Mauaji ya karibu watu 400,000. 

Hata hivyo, uhusiano kati ya viongozi hao wawili, ambao wametawala siasa za Sudan Kusini kwa miongo kadhaa, bado ni mbaya.

Kuzuiliwa nyumbani kwa Dk. Riek Machar kunaonekana kuhatarisha makubaliano ya amani.

Reath Muoch Tang, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Mahusiano ya Kigeni ya SPLM-IO, aliiambia Redio Tamazuj kwamba barua iliyotangaza kuzuiwa nyumbani kwa Machar iliwasilishwa na maafisa wakuu wa usalama, akiwemo Waziri wa Ulinzi Jenerali Chol Thon Balok.

Vikosi vya usalama vilikuja na kuwafukuza watu wote kutoka kwenye boma hilo, na waziri wa ulinzi akaondoka, lakini magari mengi ya ulinzi yalibaki kwenye boma hilo,” Reath alisema.

"Kitaalam, Dk. Machar yuko chini ya kizuizi cha nyumbani, lakini maafisa wa usalama walijaribu kumchukua," aliongeza.

Wakati huo huo, Pal Mai Deng, msemaji rasmi wa SPLM-IO, aliithibitishia Radio Tamazuj kwamba Makamu wa Kwanza wa Rais alikuwa amewekwa chini ya kizuizi cha nyumbani.

"Kwa wasiwasi mkubwa, naweza kuthibitisha kwamba Makamu wa Kwanza wa Rais na kiongozi wa SPLM/A-IO, Dk. Riek Machar, amewekwa chini ya kifungo cha nyumbani. Hii ni hatua ya kusikitisha, na hii inakiuka makubaliano ya amani yaliyohuishwa,” Pal alisema.

Pal, ambaye pia anahudumu kama Waziri wa Maji na Umwagiliaji chini ya mkataba wa kugawana madaraka, alionya kwamba uamuzi wa vikosi vya usalama na Rais Salva Kiir unadhoofisha maendeleo yaliyopatikana chini ya makubaliano ya amani ya 2018.

Amesema Dk Machar amerejea Juba kwa shinikizo la viongozi wa kikanda na kimataifa ili kuendeleza amani na utulivu nchini Sudan Kusini. 

Ameishutumu jumuiya ya kimataifa kwa kushindwa kumshinikiza Rais Kiir kutekeleza kikamilifu mkataba wa amani wa 2018.

"Jumuiya ya kimataifa ina wajibu wa kuhakikisha kwamba usalama wa kimwili wa Dk. Riek ni muhimu sana. Na hatua yoyote ambayo itahatarisha usalama wake wa kimwili itakuwa kikwazo kwa uponyaji wa kitaifa na maridhiano ya baadaye nchini Sudan Kusini," alisema.

"Taarifa alizopewa Dk. Machar ni kwamba lazima awekwe chini ya kizuizi cha nyumbani. Hata hivyo, alifahamishwa tena baadaye na maafisa hao hao wa usalama kwamba atahamishwa kutoka kwa nyumba hiyo," alihitimisha.

Msemaji wa serikali Michael Makuei hakuweza kupatikana mara moja ili kutoa maoni yake.

Vikosi vya usalama viliwekwa karibu na makazi ya Machar mapema Machi, ingawa bado aliweza kusafiri hadi ofisini kwake.

Katika kukabiliana na mapigano kaskazini mashariki mwa Jimbo la Upper Nile tangu mwishoni mwa Februari Mwaka huu, serikali ya Rais Kiir imewakamata maafisa kadhaa wa chama cha Machar, akiwemo waziri wa mafuta na petroli na naibu mkuu wa jeshi.

Rais wa Kenya William Ruto ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki amefanya mashauriano kwa njia ya simu na Rais Yoweri Museveni wa Uganda pamoja Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed ambapo baada ya Mashauri hayo amemtuma Mjumbe wake Maalum Juba nchini Sudan Kusini kwa ajili kukutana na Rais Salva Kiir Pamoja na Nakamura wake Dk.Riek Machar.

Rais Ruto ameandika kupitia ukurasa wake wa X kuwa hatua ya kumtuma Mjumbe wake Juba ni moja ya Jitihada za kutafuta suluhisho la Mgogoro baina ya Kiir na Machar na kwamba Mashaurino hayo yatatoa mwelekeo kuhusu kinachopaswa kufanyika kunusuru hali ya Mambo. 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top