UAMUZI Serikali ya Tanzania wa kuanzisha mafunzo ya jeshi la kujenga Taifa(JKT) umetajwa kuwa utaongeza uzalendo na uchungu kwa vijana katika kulitumikia na kulilinda Taifa lao.
Akisoma risala ya utii wakati wa kufunga mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria opareshini miaka 60 ya Muungano kikosi 832 KJ Ruvu mkoani Pwani,mmoja wahitimu wa mafunzo hayo Hilda Salvatory Edward,amesema pamoja na mafunzo hayo kuwafunza nidhamu, ujasiri pia yamewafanya kuwa wazalendo wa kweli kwa nchi yao.
Kwa sababu hiyo vijana hao katika risala yao hiyo pamoja na kulipongeza jeshi la kujenga taifa kupitia mkuu wa kikosi hicho,wamempongeza Rais na AMIRI jeshi mkuu mh Dr Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha uwepo wa mafunzo hayo huku wakitoa ahadi kuwa watalilinda Taifa lao na Rais wake na kamwe hawezi kwenda kushiriki katika vitendo viovu vinavyohatarisha amani ya nchi.
Naye mkuu wa kikosi cha 832 Ruvu JKT kanali Peter Elias Mnyani,amesema mafunzo hayo ya miezi mitatu kuanzia June 19 mwaka huu 2024, yameshirikisha vijana mbalimbali wakiwemo wenye ulemavu, huku akitoa wito kwa wazazi kuacha kuwaficha majumbani vijana wenye ulemavu, kwani amesema kufanya hivyo kunawanyima haki hiyo ikiwemo ya ulinzi wa Taifa lao.
Mwakilishi wa mkuu wa JKT nchini kanali George Barongo,pamoja na kumpongeza Rais Samia kuendelea kuliwezesha jeshi hilo,amesema wazo la Baba hayati Mwl Julius Kambarage la kuanzishwa kwa jeshi hilo litaendelea katika kulea na kuwajengea uzalendo vijana wa Kitanzania.
![]() |
Akizungumza wakati akifunga mafunzo hayo katika uwanja RUVU JKT maarufu kama uwanja Mabatini,mkuu wa mkoa wa Pwani,ambaye pia mwenyeki wa kamati ya Usalama ya mkoa Alhaj Aboubakar Kunenge,amewataka vijana hao kutumia fursa ya mafunzo hayo kuwa wabunifu ili kuwezesha Taifa kuondoa vijana walalamikaji.
Katika mahafali hayo ya wahitimu wa mafunzo ya jeshi la kujenga Taifa kwa mujibu wa sheria vijana wenye ulemavu wametajwa kufanya vizuri na kupewa tuzo mbalimbali.