Waitara Ahoji Wazazi wa Wabunge Kunyimwa Bima ya Afya

GEORGE MARATO TV
0


MBUNGE wa Jimbo la Tarime Vijijini mkoani Mara, Mwita Waitara, amehoji sababu zinazowazuia wazazi wa wabunge kunufaika na huduma ya Bima ya Afya inayotolewa kwa wabunge huku akiitaka Serikali kupitia upya mfumo huo ili kuleta usawa kwa familia za viongozi.

Akichangia mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Afya ya mwaka wa fedha 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma Leo Mei 12,2026 Waitara amesema kwa sasa wabunge wanapatiwa huduma ya bima kwa ajili yao, wake au waume pamoja na watoto, lakini wazazi wao hawajumuishwi kwenye mpango huo licha ya mchango mkubwa walioutoa kuwalea na kuwasomesha viongozi hao.

“Wazazi wetu walilima, walitutesa na kutusomesha mpaka tukafika hapa, lakini wanapougua mbunge analazimika kugharamia matibabu yote mwenyewe. Ni jambo linaloleta taharuki kwenye familia nyingi,” amesema Waitara.

Aidha, amewashauri viongozi wa Wizara ya Afya kutoa maelezo ya wazi kuhusu sababu za wazazi wa wabunge kutonufaika na bima hiyo, akisisitiza kuwa baadhi ya wabunge ni vijana, wajane au hawajaoa wala kuolewa hivyo wazazi wao ndio tegemeo kubwa la kifamilia.

Katika hatua nyingine, Waitara amekosoa mfumo wa “consultation fee” unaowalazimu wagonjwa kulipa fedha kabla ya kumuona daktari hospitalini, akisema hali hiyo inaongeza mzigo kwa wananchi wanaotafuta huduma za afya.

“Kwa nini mgonjwa alipe kwanza fedha ndio aeleze ugonjwa wake? Mgonjwa apewe huduma kwanza, halafu gharama nyingine zifuatilie baadaye,” amesisitiza.

Mbali na hilo, Waitara ameibua changamoto ya upungufu mkubwa wa watumishi wa afya katika vituo vya afya vya vijijini, akieleza kuwa baadhi ya maeneo yana watumishi wasiotosha licha ya Serikali kujenga majengo mazuri ya kutolea huduma.

Amevitaja vituo vya afya vya Mutanana, Bumera, Sirari, Magoma, Gibaso na Kerende kuwa miongoni mwa vituo vilivyokamilika kimajengo lakini vinakabiliwa na uhaba wa watumishi na vifaa tiba.

Pia ameishauri Serikali kukamilisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara iliyopo Musoma, akisema baadhi ya huduma muhimu ikiwemo za macho, meno, moyo na wagonjwa mahututi bado hazipatikani kutokana na mradi huo kutokukamilika.

“Wananchi wa Mara wanalazimika kwenda Bugando au Muhimbili kupata huduma hizi. Serikali ikamilishe hospitali hii ili wananchi wapate huduma karibu yao,” amesema.

Waitara ameishauri Serikali kuongeza uwekezaji katika wataalamu bingwa, vifaa tiba na huduma za afya katika vituo vya chini badala ya kuwekeza zaidi kwenye majengo pekee, akisema hatua hiyo itasaidia wananchi wengi kupata huduma bora kwa karibu.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top