Na Shomari Binda-Musoma
WANANCHI wa Jimbo la Musoma Vijijini wametoa asante kwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia fedha na kujengwa kwa shule mpya ya sekondari.
Asante na shukrani hizo zimeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Musoma Juma Chikoka,Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Profesa Sospeter Muhongo na viongozi mbalimbali walioshiriki tukio la ufunguzi wa shule mpya ya Butata sekondari leo aprili 24 2025 Kijiji cha Butata Kata ya Bukima.
Akizungumza mara baada ya kutembelea majengo ya shule hiyo yakiwemo madarasa,maabara,jengo la utawala na vyoo Chikoka amesema Rais Samia anastahili asante na shukrani.
Chikoka amesema Rais ametoa milioni 584 zilizojenga shule hiyo ambayo imewawezesha watoto kupunguza umbali mrefu wa zaidi ya kilometa 10 kwenda kwenye masomo
Amesema changamoto zilizosemwa kwenye risala likiwemo siala la umeme ametoa maagizo kwa Tanesco kuhakikisha wanafikisha huduma ya umeme ili wanafunzi waweze kusoma vizuri yakiwemo masomo ya sayansi.
" Kwa ujenzi wa shule hii hatuna budi kusema asante nyingi kwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kututhamini na kujali elimu ya watanzania.
" Uzinduzi huu ni matukio ya mfulululizo ya ufunguzi wa shule nyingine na kesho tutakuwa Kata ya Mugango lengo la serikali ni kuhakikisha shule zinakuwa karibu na wananchi na watoto wetu wanasoma bila tatizo",amesema.
Mkuu huyo wa Wilaya amemshukuru pia mbunge wa jimbo la Musoma Vijijini Profesa Sospeter Muhongo kwa ufatiliaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo ya elimu.
Amesema kama hakuna mwakilishi mzuri wa jimbo mafanikio na kupatikana kwa elimu bora hayawezi kupatikana.
Kwa upande wake mbunge Muhongo amesema kipimo kizuri cha mwakilishi ni namna anavyoshughulikia shughuli za maendeleo na kumpima kwa kazi zake.
Amesema suala la elimu bado ni kipaumbele na kumsaidia mwananchi ni kuhakikisha mtoto wake anapata elimu na kuchochea shughuli nyingine za maendeleo
Mbunge huyo amesema kwa niaba ya wananchi wanatoa asante nyingi na shukrani kwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuliona jimbo la Musoma Vijijini kwa kutoa fedha nyingi kwaajili ya miradi ikiwemo ya elimu.
Wananchi na wazazi wa wanafunzi walioshuhudia tukio hilo wametoa wito kwa wanafunzi kuhakikisha wanazingatia masomo ili wasimuanhushe Rais Samia na kuahidi kumchagua kwa kishindo kwenye uchaguzi wa 2025.