Na Emmanuel Chibasa
🚨Kila siku wanakodi jenereta na Pampu Kwa Shilingi 10,000
🚨Wanatumia kuanzia Lita 3 Hadi 20 Kwa siku Kumwagilia shamba la ekari 1 Hadi 3
🚨Lita Moja ya mafuta Bugwema inauzwa shilingi 4000
🚨Wadai Kuuziwa Pembejeo Zisizo na ubora Katika mipira ya umwagiliaji, Mbegu pamoja na dawa.
WAKULIMA wadogo wanaotegemea kilimo cha umwagiliaji kwa
kutumia Pampu zinazoendeshwa na mafuta kando kando ya ziwa Victoria, katika
kijiji cha Bugwema kata ya Bugwema Musoma Vijijini Mkoani Mara, Wanadai kutumia
gharama kubwa kutokana kukosa teknolojia nafuu, hali inayopelekea kupata hasara
na kushindwa kulima kilimo cha umwagiliaji kwa tija.
Wakulima hawa wanaeleza kuwa wamekua wakitumia fedha
nyingi kununua mafuta ya dizeli na petroli kwa ajili ya kuendesha pampu
zinazotumika kuvuta maji kutoka Ziwa Victoria. Hali hii imesababisha hasara kwa
wakulima wengi, huku wakiwa na ndoto ya kuboresha uzalishaji wao na kuleta tija
katika sekta ya kilimo cha umwagiliaji.
Wakizungumza na George Marato Tv, baadhi ya wakulima hao
wamesema kuwa, kutokana na majira ya mvua kubadirika kutokana na mabadiriko ya
tabia nchi, waliamua kuendesha shughuli za kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia
pampu za mafuta, lakini changamoto kubwa inayowakabili ni matumizi makubwa ya
fedha kwa siku ikilinganishwa na kipato wanachokipata na hivyo kushindwa
kufikia malengo waliojiwekea.
Mbali na madai ya kutumia fedha nyingi katika kuendesha
kilimo cha umwagiliaji pia wamesema hawana uelewa wa kutosha kuhusu matumizi ya
teknolojia ya nishati ya umeme jua, lakini pia kikwazo kingine ni gharama kubwa
ya kununua vifaa pamoja na upatikanaji wa wataalam kwa wakati ya kwa ajili ya
utengenezaji wa vifaa pindi vinapoharibika.
Briton Moris ni mkulima katika kijiji cha Bugwema mwenye
shamba la mahindi ekari tatu, anasema changamoto aliyonayo ni matumizi makubwa
ya kununua mafuta lita ishirini kwa siku kwa ajili ya kumwagilia ekari moja.
“Kwa siku natumia natumia lita 20 kumwagilia ekari 1 kutokana na ardhi kuwa ni mbuga ambayo inahitaji umwagiliziaji maji mengi sababu ardhi ni tepe tepe
Lakini pia hii mashine ya kumwagilia tunakodi kwa siku
shilingi elfu kumi na shida nyingine tuliyonayo ni ubovu wa mipira, Mipira
tunayonunua hudumu kabisa licha ya kununua kwa fedha nyingi” Amesema Briton
Naye Joseph Omenya ni mkulima wa bustani katika kijiji
cha Bugwema anasema licha ya kulima shamba la bustani lakini anatumia lita saba
kwa wiki kumwagilia nyanya na mboga mboga.
“Hili shamba dogo la bustani unaloliona kwa wiki natumia
lita saba kwa wiki yani ndani ya siku tatu natumia lita tatu na nusu kulingana
na ardhi tunayotumia hapa katika shughuli zetu za kilimo.
Sasa basi nawaomba wadau na serikali watusaidie kutatua
changamoto kama hizi mfano wanatakiwa kuja kutusikiliza mfano katika pembejo
pia tunaumizwa huku mshambani, unaweza kununua mbegu unajua ni mbegu ya aina
moja lakini unapofika shambani unakuta kuna aina hadi tatu za mbegu, Kwa upande
wa dawa nazo zinachakachuliwa unaweza kunyunyiza dawa shambani lakini wadudu
hawafi tunaomba serikali kudhibiti hizi bidhaa tunazonunua minadani kuhakikisha
zina ubora” Amesema Omenya.
Joseph Okaka mkulima kutoka katika kijiji cha Bugwema anaendesha shughuli za kilimo kandokando ya ziwa victoria anaeleza kuwa katika shamba la mahindi alilolima kwa siku amekua akitumia lita tatu kwa siku kumwagilia na changamoto nyingine kubwa anayopata ni gharama za matengezo inapotokea Pump imeharibika.
“Ndugu mwandishi hapa katika kijiji cha bugwema lita
moja ya mafuta ni shilingi 4,000/= kwa lita moja na katika shamba langu natumia
lita tatu kwa siku ambayo ni sawa na shilingi 12,000/= na bado nalipia shilingi
10,000/= ambayo ni gharama ya kukodi genereta na uharibifu wowote unapotokea
kwenye Pump au jenereta gharama zinakua juu yangu.
Naiomba serikali iweze kutuangalia na kutusidia sisi
wakulima wadogo kwa kutuwezesha vifaa vya solar ili tuweze kuondokana na
changamoto hizi lakini pia makampuni ya solar yaje kutupa elimu ili tuweze kuwa
na uelewa wa kutosha juu ya teknolojia hii sababu hakuna kampuni hata moja
imefika hapa na kutoa elimu hii kwa wakulima na wananchi “ Amesema Okaka
Loyce Joshua ambaye pia ni mkulima wa shamba la mboga mboga anasema pia anatumia mafuta lita tatu kumwagilia shamba lake, na katika shughuli hiyo anaona bado hajapata mafanikio kutokana na kilimo cha umwagiliaji na kueleza kuamini matumizi ya kumwagilia kwa kutumia solar yanaweza kumsaidia kupata faida huku Penina Elisha akieleza kuwa ameshindwa kumudu kulima shamba kubwa kutokana na kukosa fedha kwa ajili ya kumwagilia kwa kutumia pampu.
“Mimi hapa nalima shamba kidogo sababu nasomba maji kwa
mikono na maji hayapo jirani na shamba, lakini endapo nitawezeshwa na serikali
kwa kupata miundombinu ya solar kwa ajili ya kumwagilia nitaweza kulima shamba
kubwa na kupata faida” Amesema Penina.
Mbali na changamoto ya kutumia gharama kubwa katika
kukodi pampu, jenereta pamoja na kununua mafuta, changamoto nyingine
inayowakabili wanadai pia kuletewa pembejeo ambazo hazina ubora hususani mipira
inayotumika kwenye Pampu za mafuta kumwagilizia, mbegu na madawa feki pamoja na
mahindi yao kuharibiwa na ndege pindi yanapoanza kukomaa kama wanavyoeleza Joseph
Omenya
“Tunaomba serikali na wadau wa kilimo watusaide unakuta
unanunua mbegu imeandikwa jina moja lakini ukifika shambani kupanda unakuta
kuna aina tatu za mbegu kwenye kifungashio kimoja, Kwa upande wa dawa nazo
asilimia kubwa zimechakachuliwa unaweza ukanunua na kupuliza dawa kwenye
mashamba yetu lakini haziuwi wadudu sasa tunashindwa kuelewa kama dawa kweli
zimethibitishwa kwa nini hawapiti kufuatilia dawa tunauziwa huku vijijini”
Amasema Omenya
Kwa upande wake Kefa Lucas mkulima wa mahindi, anasema
kwa sasa amesitisha kufanya shughuli za maendeleo na anashindia shambani
kulinda ndege ambao kwa sasa wamekua tishio katika kuharibu mazao yao.
“Tunategemea kulima eneo kubwa ili nipate mavuno mengi lakini ndege wamekuwa ni tatizo mpaka inatubidi tutumie chupa za plastiki kuweka kwenye mahindi ili ndege wasiharibu lakini bado ndege wanaharibu mahindi yetu hivyo naiomba serikali itusaidie kudhibiti hawa ndege ili tupate mavuno mengi” Anasema Kefa.
Kwa upande wake afisa mtendaji wa kijiji cha Bugwema Daud
Zacharia anesema wakulima hao wanatumia gharama kubwa katika kilimo cha
umwagiliaji kwa kutumia pampu za mafuta kutokana na kukosa miundombinu ya
umwagiliaji kwa kutumia nishati ya umeme jua.
Anasema ardhi katika kijiji cha Bugwema inafaa kwa ajili
ya kilimo cha umwagiliaji lakini wakulima wanakosa elimu ya matumizi ya vifaa
vya solar ili waweze kufahamu faida na kuwezesha kuhama kutoka matumizi ya
pampu za mafuta na kutumia solar.
“Naomba wadau hususani haya makampuni ya Solar waje kutoa elimu kwa wakulima lakini kuangalia namna ya kuwawezesha wakulima kulima kilimo chenye tija na kuweza kuleta maendeleo katika jamii.
Pia naiomba serikali kuendelea kuwadhibiti
wafanyabishara wanaingiza nchini bidhaa zisizo na ubora pamoja na pembejeo zisizo
na ubora kwani zimekua zikirudisha nyuma jitihada za maendeleo kwa wakulima
wanaojihusisha na kilimo cha umwagiliaji na kushindwa kulima kwa tija.” Amesema
Zacharia
Elizabeth Komanyani mtaalam wa nishati ya umeme jua ambaye pia ni afisa masoko wa kampuni Simu Solar Tanzania, anathibitisha kuwa Pampu za umeme jua zinaweza kusaidia wakulima wadogo kwa gharama nafuu na zisizo na madhara kwa mazingira na ni bora kwa wakulima wadogo kwa sababu hazihitaji gharama za kila siku kama za mafuta.
Anasema Solar pampu ni uwekezaji wa mara moja, na mkulima anaweza kuzihamisha kwa urahisi kutoka shamba moja hadi jingine na matumizi ya teknolojia hii yanaweza kusaidia wakulima kuongeza uzalishaji na kutokomeza umasikini.
Wakulima wa kilimo cha umwagiliaji kabla ya kununua
vifaa vya solar wanapaswa kuwaona wataalam ili kutembelea maeneo yao ili
kuangalia pia vyanzo vya maji ili kushauri pampu za solar zinazotakiwa
kutumika.
“ Kuna aina mbili za solar kwa ajili ya kilimo cha
umwagiliaji, kuna pampu zinazotumika katika maji ya visima lakini pia kuna
pampu ambazo vyanzo vyake vya maji ni ziwa, mabwawa au mito.
Pia kabla ya sisi kumuuzia mteja pampu lazima pia
tuangalie wingi wa maji katika eneo lake pamoja na mazao gani ambayo mkulima
anatarajia kulima, yani tunauza kwa kutegemea mahitaji ya mteja kulingana na
ekari za mkulima anazokusudia kulima.
Pia katika kuwafikia wakulima wengi tumeweka utaratibu kwa wakulima kulipa malipo yote kwa mara moja lakini pia kwa kulipa kidodogo kwa malipo ya kila mwezi ili kumsaidia mkulima kuondokana na mtumizi ya pampu za mafuta” Amesema Elizabeth
Upatikanaji wa nishati ya umeme jua(solar) kwa matumizi
ya wanadamu ni moja ya huduma muhimu na ya msingi kwa maisha na ustawi wa
wanadamu. Kulingana na Sera ya Nishati ya 2015 ya Tanzania, serikali ina wajibu
wa kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya umeme, ikiwa ni pamoja na umeme jua,
kwa wananchi wa vijijini.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa mwaka 2023 na wizara
ya kilimo, inaeleza kuwa Serikali
imepanga kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo kwa kuelekeza rasilimali zaidi
kwenye ujenzi wa miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji.
Taarifa hiyo iliyo tolewa na aliyekua Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Anthony Mavunde (Mb) wakati akizungumza kwenye Mkutano wa Wafanyabiashara na wadau wanaouza mazao ya kilimo ndani na nje ya nchi uliofanyika tarehe 14 Julai 2023, jijini Dodoma.
Mhe. Mavunde alisesema kuwa katika bajeti ya mwaka wa
fedha 2023/24, Serikali imeweka mkakati wa kujenga mabwawa 100 nchi nzima yenye uwezo wa kuhifadhi lita bilioni 900 nchi
nzima. Ameongeza kuwa Serikali itachimba
visima 150 katika kila halmashauri kwa
ajili ya kilimo cha umwagiliaji.
Maeneo yenye vyanzo vya maji, hususani mito na maziwa,
Serikali imepanga kujenga miundombinu itakayofikisha maji kwenye mashamba ya
wakulima.
Aidha, mabonde yote nchini yatafanyiwa upembuzi yakinifu ambapo hekta 3,016,600 zitapatikana na kuwekewa
miundomninu kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.
Mhe. Mavunde aliyataja mabonde hayo kuwa bonde la ziwa
Viktoria, Bugwema, Suguti, Mto Ngono, Manga Homere, Ngomai na litumbandios.
Mabonde mengine ni Mto Ruvuma, Mto Songwe, Ifakara
Idete, Rufiji ya Chini, Kilombero, Mkomazi na
Pangani.
Mradi wa bonde la Bugwema na Suguti katika halmashauri ya Musoma vijijini ukikamilika utasaidia kutatua changamoto za wakulima wadogo zinazowakabili ikiwa ni pamoja na matumizi ya nishati ya jua kama mkakati wa kupunguza gharama za uendashaji katika kilimo cha umwagiliaji.
Picha ya Briton Moris ni mkulima katika kijiji cha Bugwema mwenye shamba la mahindi ekari tatu
Picha ya Mkulima Goldon wa kijiji cha Bugwema mwenye shamba la mahindi akieleza changamoto katika kilimo cha umwagiliaji.


























