Wakulima Bugwema Waeleza Jinsi Kilimo cha Umwagiliaji Kwa Kutumia Pampu za Mafuta Kinavyowapa Hasara

GEORGE MARATO TV
0


Na Emmanuel Chibasa

🚨Kila siku wanakodi jenereta na Pampu Kwa Shilingi 10,000

🚨Wanatumia kuanzia Lita 3 Hadi 20 Kwa siku Kumwagilia shamba la ekari 1 Hadi 3

🚨Lita Moja ya mafuta Bugwema inauzwa shilingi 4000

🚨Wadai Kuuziwa Pembejeo Zisizo na ubora Katika mipira ya umwagiliaji, Mbegu pamoja na dawa.


WAKULIMA wadogo wanaotegemea kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia Pampu zinazoendeshwa na mafuta kando kando ya ziwa Victoria, katika kijiji cha Bugwema kata ya Bugwema Musoma Vijijini Mkoani Mara, Wanadai kutumia gharama kubwa kutokana kukosa teknolojia nafuu, hali inayopelekea kupata hasara na kushindwa kulima kilimo cha umwagiliaji kwa tija.

Wakulima hawa wanaeleza kuwa wamekua wakitumia fedha nyingi kununua mafuta ya dizeli na petroli kwa ajili ya kuendesha pampu zinazotumika kuvuta maji kutoka Ziwa Victoria. Hali hii imesababisha hasara kwa wakulima wengi, huku wakiwa na ndoto ya kuboresha uzalishaji wao na kuleta tija katika sekta ya kilimo cha umwagiliaji.

Wakizungumza na George Marato Tv, baadhi ya wakulima hao wamesema kuwa, kutokana na majira ya mvua kubadirika kutokana na mabadiriko ya tabia nchi, waliamua kuendesha shughuli za kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia pampu za mafuta, lakini changamoto kubwa inayowakabili ni matumizi makubwa ya fedha kwa siku ikilinganishwa na kipato wanachokipata na hivyo kushindwa kufikia malengo waliojiwekea.

Mbali na madai ya kutumia fedha nyingi katika kuendesha kilimo cha umwagiliaji pia wamesema hawana uelewa wa kutosha kuhusu matumizi ya teknolojia ya nishati ya umeme jua, lakini pia kikwazo kingine ni gharama kubwa ya kununua vifaa pamoja na upatikanaji wa wataalam kwa wakati ya kwa ajili ya utengenezaji wa vifaa pindi vinapoharibika.

Briton Moris ni mkulima katika kijiji cha Bugwema mwenye shamba la mahindi ekari tatu, anasema changamoto aliyonayo ni matumizi makubwa ya kununua mafuta lita ishirini kwa siku kwa ajili ya kumwagilia ekari moja.

“Kwa siku natumia natumia lita 20 kumwagilia ekari 1 kutokana na ardhi kuwa ni mbuga ambayo inahitaji umwagiliziaji maji mengi sababu ardhi ni tepe tepe

Lakini pia hii mashine ya kumwagilia tunakodi kwa siku shilingi elfu kumi na shida nyingine tuliyonayo ni ubovu wa mipira, Mipira tunayonunua hudumu kabisa licha ya kununua kwa fedha nyingi” Amesema Briton

Naye Joseph Omenya ni mkulima wa bustani katika kijiji cha Bugwema anasema licha ya kulima shamba la bustani lakini anatumia lita saba kwa wiki kumwagilia nyanya na mboga mboga.

“Hili shamba dogo la bustani unaloliona kwa wiki natumia lita saba kwa wiki yani ndani ya siku tatu natumia lita tatu na nusu kulingana na ardhi tunayotumia hapa katika shughuli zetu za kilimo.

Sasa basi nawaomba wadau na serikali watusaidie kutatua changamoto kama hizi mfano wanatakiwa kuja kutusikiliza mfano katika pembejo pia tunaumizwa huku mshambani, unaweza kununua mbegu unajua ni mbegu ya aina moja lakini unapofika shambani unakuta kuna aina hadi tatu za mbegu, Kwa upande wa dawa nazo zinachakachuliwa unaweza kunyunyiza dawa shambani lakini wadudu hawafi tunaomba serikali kudhibiti hizi bidhaa tunazonunua minadani kuhakikisha zina ubora” Amesema Omenya.

Joseph Okaka mkulima kutoka katika kijiji cha Bugwema anaendesha shughuli za kilimo kandokando ya ziwa victoria anaeleza kuwa katika shamba la mahindi alilolima kwa siku amekua akitumia lita tatu kwa siku kumwagilia na changamoto nyingine kubwa anayopata ni gharama za matengezo inapotokea Pump imeharibika.

“Ndugu mwandishi hapa katika kijiji cha bugwema lita moja ya mafuta ni shilingi 4,000/= kwa lita moja na katika shamba langu natumia lita tatu kwa siku ambayo ni sawa na shilingi 12,000/= na bado nalipia shilingi 10,000/= ambayo ni gharama ya kukodi genereta na uharibifu wowote unapotokea kwenye Pump au jenereta gharama zinakua juu yangu.

Naiomba serikali iweze kutuangalia na kutusidia sisi wakulima wadogo kwa kutuwezesha vifaa vya solar ili tuweze kuondokana na changamoto hizi lakini pia makampuni ya solar yaje kutupa elimu ili tuweze kuwa na uelewa wa kutosha juu ya teknolojia hii sababu hakuna kampuni hata moja imefika hapa na kutoa elimu hii kwa wakulima na wananchi “ Amesema Okaka

Loyce Joshua ambaye pia ni mkulima wa shamba la mboga mboga anasema pia anatumia mafuta lita tatu kumwagilia shamba lake, na katika shughuli hiyo anaona bado hajapata mafanikio kutokana na kilimo cha umwagiliaji na kueleza kuamini matumizi ya kumwagilia kwa kutumia solar yanaweza kumsaidia kupata faida huku Penina Elisha akieleza kuwa ameshindwa kumudu kulima shamba kubwa kutokana na kukosa fedha kwa ajili ya kumwagilia kwa kutumia pampu.

“Mimi hapa nalima shamba kidogo sababu nasomba maji kwa mikono na maji hayapo jirani na shamba, lakini endapo nitawezeshwa na serikali kwa kupata miundombinu ya solar kwa ajili ya kumwagilia nitaweza kulima shamba kubwa na kupata faida” Amesema Penina.

Mbali na changamoto ya kutumia gharama kubwa katika kukodi pampu, jenereta pamoja na kununua mafuta, changamoto nyingine inayowakabili wanadai pia kuletewa pembejeo ambazo hazina ubora hususani mipira inayotumika kwenye Pampu za mafuta kumwagilizia, mbegu na madawa feki pamoja na mahindi yao kuharibiwa na ndege pindi yanapoanza kukomaa kama wanavyoeleza Joseph Omenya

“Tunaomba serikali na wadau wa kilimo watusaide unakuta unanunua mbegu imeandikwa jina moja lakini ukifika shambani kupanda unakuta kuna aina tatu za mbegu kwenye kifungashio kimoja, Kwa upande wa dawa nazo asilimia kubwa zimechakachuliwa unaweza ukanunua na kupuliza dawa kwenye mashamba yetu lakini haziuwi wadudu sasa tunashindwa kuelewa kama dawa kweli zimethibitishwa kwa nini hawapiti kufuatilia dawa tunauziwa huku vijijini” Amasema Omenya


Kwa upande wake Kefa Lucas mkulima wa mahindi, anasema kwa sasa amesitisha kufanya shughuli za maendeleo na anashindia shambani kulinda ndege ambao kwa sasa wamekua tishio katika kuharibu mazao yao.

“Tunategemea kulima eneo kubwa ili nipate mavuno mengi lakini ndege wamekuwa ni tatizo mpaka inatubidi tutumie chupa za plastiki kuweka kwenye mahindi ili ndege wasiharibu lakini bado ndege wanaharibu mahindi yetu hivyo naiomba serikali itusaidie kudhibiti hawa ndege ili tupate mavuno mengi” Anasema Kefa.

Kwa upande wake afisa mtendaji wa kijiji cha Bugwema Daud Zacharia anesema wakulima hao wanatumia gharama kubwa katika kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia pampu za mafuta kutokana na kukosa miundombinu ya umwagiliaji kwa kutumia nishati ya umeme jua.

Anasema ardhi katika kijiji cha Bugwema inafaa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji lakini wakulima wanakosa elimu ya matumizi ya vifaa vya solar ili waweze kufahamu faida na kuwezesha kuhama kutoka matumizi ya pampu za mafuta na kutumia solar.

“Naomba wadau hususani haya makampuni ya Solar waje kutoa elimu kwa wakulima lakini kuangalia namna ya kuwawezesha wakulima kulima kilimo chenye tija na kuweza kuleta maendeleo katika jamii.

Pia naiomba serikali kuendelea kuwadhibiti wafanyabishara wanaingiza nchini bidhaa zisizo na ubora pamoja na pembejeo zisizo na ubora kwani zimekua zikirudisha nyuma jitihada za maendeleo kwa wakulima wanaojihusisha na kilimo cha umwagiliaji na kushindwa kulima kwa tija.” Amesema Zacharia

Elizabeth Komanyani mtaalam wa nishati ya umeme jua ambaye pia ni afisa masoko wa kampuni Simu Solar Tanzania, anathibitisha kuwa Pampu za umeme jua zinaweza kusaidia wakulima wadogo kwa gharama nafuu na zisizo na madhara kwa mazingira na ni bora kwa wakulima wadogo kwa sababu hazihitaji gharama za kila siku kama za mafuta.

Anasema Solar pampu ni uwekezaji wa mara moja, na mkulima anaweza kuzihamisha kwa urahisi kutoka shamba moja hadi jingine na matumizi ya teknolojia hii yanaweza kusaidia wakulima kuongeza uzalishaji na kutokomeza umasikini.


Wakulima wa kilimo cha umwagiliaji kabla ya kununua vifaa vya solar wanapaswa kuwaona wataalam ili kutembelea maeneo yao ili kuangalia pia vyanzo vya maji ili kushauri pampu za solar zinazotakiwa kutumika.

“ Kuna aina mbili za solar kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji, kuna pampu zinazotumika katika maji ya visima lakini pia kuna pampu ambazo vyanzo vyake vya maji ni ziwa, mabwawa au mito.

Pia kabla ya sisi kumuuzia mteja pampu lazima pia tuangalie wingi wa maji katika eneo lake pamoja na mazao gani ambayo mkulima anatarajia kulima, yani tunauza kwa kutegemea mahitaji ya mteja kulingana na ekari za mkulima anazokusudia kulima.

Pia katika kuwafikia wakulima wengi tumeweka utaratibu kwa wakulima kulipa malipo yote kwa mara moja lakini pia kwa kulipa kidodogo kwa malipo ya kila mwezi ili kumsaidia mkulima kuondokana na mtumizi ya pampu za mafuta” Amesema Elizabeth

Upatikanaji wa nishati ya umeme jua(solar) kwa matumizi ya wanadamu ni moja ya huduma muhimu na ya msingi kwa maisha na ustawi wa wanadamu. Kulingana na Sera ya Nishati ya 2015 ya Tanzania, serikali ina wajibu wa kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya umeme, ikiwa ni pamoja na umeme jua, kwa wananchi wa vijijini.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa mwaka 2023 na wizara ya kilimo, inaeleza kuwa  Serikali imepanga kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo kwa kuelekeza rasilimali zaidi kwenye ujenzi wa miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji.

Taarifa hiyo iliyo tolewa na aliyekua Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Anthony Mavunde (Mb) wakati akizungumza kwenye Mkutano wa Wafanyabiashara na wadau wanaouza mazao ya kilimo ndani na nje ya nchi uliofanyika tarehe 14 Julai 2023, jijini Dodoma. 

Mhe. Mavunde alisesema kuwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2023/24, Serikali imeweka mkakati wa kujenga  mabwawa 100 nchi nzima yenye  uwezo wa kuhifadhi lita bilioni 900 nchi nzima.  Ameongeza kuwa Serikali itachimba visima 150 katika kila halmashauri kwa  ajili ya kilimo cha umwagiliaji.

Maeneo yenye vyanzo vya maji, hususani mito na maziwa, Serikali imepanga kujenga miundombinu itakayofikisha maji kwenye mashamba ya wakulima.

Aidha, mabonde yote nchini  yatafanyiwa upembuzi yakinifu  ambapo hekta 3,016,600 zitapatikana na kuwekewa miundomninu kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.

Mhe. Mavunde aliyataja mabonde hayo kuwa bonde la ziwa Viktoria, Bugwema, Suguti, Mto Ngono, Manga Homere, Ngomai na  litumbandios.

Mabonde mengine ni Mto Ruvuma, Mto Songwe, Ifakara Idete, Rufiji ya Chini, Kilombero, Mkomazi na  Pangani.

Mradi wa bonde la Bugwema na Suguti katika halmashauri ya Musoma vijijini ukikamilika utasaidia kutatua changamoto za wakulima wadogo zinazowakabili ikiwa ni pamoja na matumizi ya nishati ya jua kama mkakati wa kupunguza gharama za uendashaji katika kilimo cha umwagiliaji.


Picha ya Briton Moris ni mkulima katika kijiji cha Bugwema mwenye shamba la mahindi ekari tatu

 

Picha ya Mkulima Goldon wa kijiji cha Bugwema mwenye shamba la mahindi akieleza changamoto katika kilimo cha umwagiliaji.

Picha ya mkulima Loyce Joseph mkulima wa shamba la mboga mboga mboga  kijiji cha Bugwema akizungumza changamoto za kilimo


Picha ya mkulima Penina Marcus  mkulima wa shamba la mboga mboga mboga  kijiji cha Bugwema akizungumza changamoto za kilimo

Picha ya mkulima Kefa Lucas Akieleza changamoto anazopata Katika kilimo cha umwagiliaji na jinsi ndege wanavyoharibu shamba lake la mahindi.


Picha ya mkulima Joseph Omenya wa Kijiji cha Bugwema akieleza jinsi changamoto ya pembejeo zisizo na ubora ikiwa ni pamoja na mbegu na madawa ya kilimo feki yanavyowapa hasara katika kilimo cha umwgiliaji.

Picha ya mkulima katika kijiji cha Bugwema akimwagilia shamba lake la mboga mboga kwa kutumia mikono kutokana na kutomudu gharama za kukodi pampu ya mafuta, genereta pamoja na kununua mafuta kila siku kumwgilia shamba lake.


Picha ya wakulima Kefa Lucas,Briton Moris Pamoja na Joseph Okaka wakionesha mpira wa kumwagilizia kwa kutumia pampu ya mafuta ukiwa umetoboka baada ya kuutumia kwa kipindi cha miezi miwili tu na wameununua kwa shilinigi 250,000/=

Picha ya mtendaji wa Kijiji cha Bugwem Daud Zacharia akieleza mkakati wa serikali katika mradi wa bonde la Bugwema pamoja na kueleza adha wanazopata wakulima kutokana na kumwagilia mazao yao kwa kutumia pampu za mafuta


Picha ya mtaalam wa nishati ya umeme jua na afisa masoko wa kampuni ya Simu Solar Tanzania Elizabeth Komanya akitoa maelezo jinsi nishati ya umeme jua inavyo fanya kazi katika kilimo cha umwagiliaji na faida zake katika kupunguza gharama wanazotumia wakulima kwa kumwagilia kwa pampu za mafuta.

Picha ya Shamba la mahindi katika kijiji cha bugwema ambapo mahindi ambayo yameanza kukomaa yakiwa yamewekewa chupa za Plastiki ili yasiharibiwe na ndege.

Picha ya Mhindi ukiwa umeharibiwa na ndege ukiwa bado shambani katika kijiji cha Bugwema Musoma Vijijini

Picha ya Paneli za Solar zinazofaa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji

Picha ya shamba la mahindi yanayo mwagiliwa kwa pampu ya mafuta katika kijiji cha bugwema

Picha ya wakulima wakiwa katika shaamba la nyanya katika kijiji cha Bugwema Musoma Vijijini


Picha za pampu za umwagiliaji kwa kutumia nishati ya umeme jua kutoka kampuni ya Simu Solar Tanzania





Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top