NA MWANDISHI WETU;NIRC KAGERA
Serikali ina mpango wa kujenga soko la kisasa la ndizi Mkoani Kagera ili kuwasaidia wakulima Mkoani humo kupata bei nzuri ya mazao yao.
Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Kilimo David Silinde wakati wa kuhitimisha Maonesho ya wiki ya chakula duniani yaliyofanyika kitaifa mkoani kagera.
Silinde pia amewataka washiriki wote wa maonyesho hayo kuzingatia mambo waliyojifunza ili kuboresha uzalishaji na hivyo kuwa na uhakika wa chakula na lishe kwa jamii.
Awali Naibu Waziri Silinde ametembelea mabanda ya washiriki wa maonyesho hayo likiwemo banda la Tume ya Taifa ya Umwagiliaji na na kusifu hatua zinazochukuliwa katika utekelezaji wa miradi.
Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Uendeshaji kutoka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Salome Njau, amesema kuwa maonyesho hayo yamekuwa na mafanikio makubwa kwa upande wa Tume hiyo.
Salome amesema kuwa wameweza kuhudumia wakulima zaidi ya 200 na kutoa elimu ya mbinu bora za kilimo cha umwagiliaji ili waweze kulima kwa ajili ya chakula na biashara kwa ujumla.
Kwa mujibu wa Salome,Tume ya Taifa ya Umwagiliaji tayari imetangaza zabuni kwa ajili ya uchimbaji wa visima vinne ambavyo vitawezesha baadhi ya wakulima Mkoa wa Kagera kuondokana na kilimo cha kutegemea mvua na hivyo kuongeza tija.